|
|
 |
 |
Historia yetu kwa ufupi
Matangazo ya kwanza Matangazo ya mwanzo kabisa ya Idhaa ya Kiswahili ya BBC yalitangazwa hewani Juni 27 mwaka wa 1957. Mtangazaji wa kwanza alikuwa marehemu Oscar Kambona ambaye baadae alikuja kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Nje wa Tanganyika na baadaye Tanzania. Katika miaka ya mwanzo mwanzo, matangazo hayo yalikuwa ya dakika 15 peke yake na yalichukuwa nafasi muhimu katika nchi changa zilizokuwa zinainukia katika Afrika Mashariki.
Marais wapigania uhuru Marais wa kwanza wa Tanzania na Kenya, marehemu Mzee Jomo Kenyatta na Mwalimu Julius Nyerere, mara kwa mara walikuwa wageni mashuhuri kwenye vipindi vya habari wakati walipokuwa wakipigania uhuru wa nchi zao.
Habari na Matukio Tangu wakati huo Idhaa hii imeendelea kuwahoji viongozi mashuhuri wa kisiasa katika sehemu hiyo, pamoja na kuripoti habari na matukio muhimu Afrika Mashariki na Kati na duniani kote. Matangazo yote yamekuwa yakipeperushwa kutoka London na wakati mwingine huwa tunaungana na studio zetu za Nairobi.
Taarifa sahihi Kwa kipindi cha zaidi ya miaka 40 sasa Idhaa yetu imekuwa ikijipatia sifa kemkem kwa kutangaza habari sahihi na motomoto. Kwa mfano Idhaa hii ilikuwa ya kwanza kutangaza taarifa za mauaji ya Dr. Robert Ouko katika mwaka 1990, pamoja na ajali ya ndege iliyowaua Rais Juvenile Habyarimana wa Rwanda na Rais Cyprien Ntayamira wa Burundi mnamo mwaka 1994.
Pia tuliweza kutangaza moja kwa moja kutoka Afrika Mashariki wakati wa uchaguzi wa vyama vingi katika nchi hizo. Kwa mfano, huko Kenya (1992 na 1997), Msumbiji (1994, na 1999), Malawi (1994 na 2000), Tanzania (1995 na 2000), Uganda (1996). Vile vile Idhaa hii ilitangaza taarifa za kuugua, kufariki kwa Mwalimu Julius Nyerere katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas hapa London na kisha kusafirishwa hadi Dar es Salaam kwa mwili wa Rais huyo wa kwanza wa Tanzania.
Mahojiano maalum Mwishoni mwa mwaka 2000, tulikuwa na mahojiano maalumu na marehemu Laurent Desire Kabila, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kwa kipindi cha miaka minne. Haya yalikuwa mazungumzo ya mwisho kabisa aliyoyafanya na mwandishi wa Habari kabla ya kuuawa kwa kupigwa risasi.
Wasikilizaji milioni 10 Kwa sasa Idhaa hii inatangaza kwa muda wa masaa mawili na robo kwa siku, (ikiwa ni pamoja na matangazo kwa. Wasikilizaji wetu wa Afrika ya Kati) au masaa kumi na tano kwa wiki kutoka studio zetu za Bush House, London na Nairobi. Matangazo yetu yanawafikia zaidi ya zaidi ya wasikilizaji milioni kumi kwa wiki.
Matangazo kwenye mtandao (Online) Maendeleo ya teknolojia katika dunia na hasa katika nyanja ya habari na mawasiliano yameiwezesha Idhaa ya Kiswahili kukuletea matangazo ya moja kwa moja katika mtandao wa kompyuta. Unaweza kusikiliza matangazo yetu yote kwa muda wa masaa 24. Bonyeza: www.bbc.co.uk/swahili. Pia unaweza kutuma maoni yako kwa kutumia email.
Wasiliana nasi kwa njia ya e-mail: swahili@bbc.co.uk
|
|
 |
 |
|
|
 |
 |
 |
 |
 |
 |
 |
|
|
| BBC haina dhamana juu ya yale yaliyoandikwa katika kurasa za internet za mashirika mengine |
 |
| Wasiliana Nasi |
 |
| Email:swahili@bbc.co.uk |
 |
Au tuandikie Bush House, Strand, London WC2B 4PH |
Tel: + 44 207 557 2502 Fax: + 44 207 240 4637
|
|