14 Juni, 2004 - Imetolewa 11:11 GMT
Kipindi cha Kimasomaso kilianzishwa kwa lengo la kujadili maswala yanayowahusu vijana kama vile afya ya uzazi na mengineyo kwa ujumla.
Kimasomaso kimekuwa maarufu miongoni mwa wasikilizaji wetu kutokana na ukweli kwamba kimekuwa kikijadili mambo yanayowagusa katika maisha ya kila siku.
Kimasomaso, ukweli wa mambo, ukweli halisi, ukweli usio na kificho ni kipindi kinachowahusu hasa vijana wa rika mbalimbali. Matarajio ni kuwa jamii nzima itaweza kujifunza mengi kutoka kwenye makala haya. Makala ambayo yanayakabili maswala yanayowahusu vijana kwa uwazi sana labda kuliko ilivyo wahi kutokea huko nyuma.
Vijana wenyewe wanazungumza kuhusu ni kwanini wanatumia madawa ya kulevya, kwanini wanakuwa makahaba , kwanini wanapata mimba wakiwa wadogo, kwanini wanakabiliwa vibaya na ugonjwa wa ukimwi, kwanini iwe hivi na vile. Lakini baada ya yote, tarajio kubwa ni kwamba tupate funzo litakaloisaidia jamii kukabiliana na matatizo haya.
Madawa ya kulevya
Tatizo la matumizi ya madawa ya kulevya linazidi kukithiri. Pamoja na juhudi kubwa za kuyadhibiti, hali ya utumiaji, ununuzi na uuzaji wa madawa ya kulevya hasa madawa makali makali kama vile cocaine na heroine yakijulikana vyema huko mitaani kama unga , pamoja na bangi inaelekea kuvuka mpaka.
Ukahaba
Uuzaji wa mapenzi , uchangudoa , ukahaba au umalaya ni biashara ya tangu jadi… lakini ukweli ni kwamba jamii, hasa ya kiafrika, katu haijaikubali biashara hii. Matokeo yake ni wasichana hao kubaguliwa, bila watu kutaka kujua kiini cha tatizo na ufumbuzi wake … ili kutumulikia picha halisi ya yale wanayoyapitia kila siku katika kazi hio ya uchangudoa tumekuwa nae msichana Zena kutoka Dar Es salaam.
Maisha ya ndoa
Vijana wawili John na Catherine ambao walikutana katika matatu mjini Nairobi, wakapendana na kuamua kufunga pingu za maisha ni miongoni tu wa wahusika wetu katika kipindi.
Watangazaji
Mtangazaji wa kipindi cha Kimasomaso ni Tom Japanni akishirikiana na Amina Aboubakar.
Wasiliana nasi
Kama nawe unayo ya kutuambia , kuhusu maisha yako au ukiwa na maoni kuhusu kipindi hiki unaweza kutuandikia kwa kutumia anuani
yetu ya e-mail ambayo ni kimasomaso@bbc.co.uk, au tuma text message kwa namba hii 000 44 77 86 202 005, au tupigie simu namba
250 744 Nairobi ama tuandikie barua kwa kutumia sanduku la barua 58621, Nairobi.